Thursday, January 18, 2018

MAAZIMIO YA MKUTANO KATI YA SMZ NA SMT KUSHUGHULIKIA MELI ZINAZOPEPERUSHA BENDERA YA TANZANIA KWA TUHUMA ZA KUSAFIRISHA SILAHA NA MADAWA YA KULEVYA, TAREHE 17 JANUARI 2018

Ndugu Waandishi wa Habari, nimewaita hapa kuzungumza nanyi na kupitia kwenu kuzungumza na wananchi wenzangu kuhusu taaarifa ya kukamatwa kwa meli zilizokuwa zimepakia shehena za dawa za kulevya na silaha zikiwa zinapeperusha bendera ya nchi yetu.


Meli hizo ni: 

Kaluba yenye usajili namba IMO 6828753 iliyokamatwa tarehe 27 Desemba 2017 ikiwa na wastani wa kilo 1,600 za dawa za kulevya huko katika maeneo ya Jamhuri ya Dominican Republic; na 

Andromeda yenye namba za usajili IMO 7614666 iliyokamatwa kwa kusafirisha silaha kinyume na Sheria za kimataifa. 

Meli zote mbili zimesajiliwa Tanzania kupitia taasisi yetu ya Mamlaka ya Usafiri Baharini Zanzibar ambayo ndiyo imepewa mamlaka ya kusajili meli za nje.

Hapa kwetu Tanzania tuna aina mbili za kusajili Meli; usajili wa Meli zenye asili ya Tanzania na zile zenye asili ya Nje. kwa kuzingatia kuwa Tanzania ni nchi mwanachama wa Umoja wa Mataifa na mashirika yake mbalimbali, siku zote tumekuwa tunaheshimu na kutekeleza kikamilifu majukumu yetu ya kimataifa yaliyowekwa kupitia mikataba na maazimio mbalimbali ya vyombo hivyo

Ndugu Waandishi wa Habari, kwa mujibu wa mkataba wa UNCLOS 1982 kila nchi imepewa haki ya kufanya usajili wa meli kwa kuzingatia mikataba ya kimataifa na sheria za nchi husika.Kwa upande wa Tanzania, usajili wa meli za kimataifa unasimamiwa na Sheria Na 5 ya mwaka 2006,


(Kwa upande wa SUMATRA ina Merchant Shipping Act ya mwaka 2003. Sheria hi inaruhusu usajili wa meli inayomilikiwa na Mtanzania, au meli inayomilikiwa kwa ubia kati ya Mtanzania na raia wa nchi nyingine. Kwa sheria hii ili meli ipate usajili wa SUMATRA na kuruhusiwa kupeperusha bendera ya Tanzania ni lazima umiliki wa meli uhusishwe na raia wa Tanzania kwa umiliki wote au kwa ubia lakini ni lazima Mtanzania awe na hisa nyingi. Vilevile kampuni hiyo ya umiliki lazima iwe ya Kitanzania kwa maana ya kusajiliwa na kujiendesha kutokea Tanzania hata kama kampuni hiyo inamilikiwa na watu wasio Watanzania. Na kwa upande wa Zanzibar kupitia ZMA wana Maritime Transport Act ya mwaka 2006).

Sheria hii inaruhusu usajili wa meli yoyote hata kama mmiliki wake sio Mtanzania wala kampuni kuwa ya Kitanzania hivyo basi kutoa fursa kwa meli ambayo haina umiliki wa aina yeyote wa Tanzania kwa maana umiliki na ukazi kupewa usajili wa kupeperusha bendera yetu nje ya Tanzania. Aidha, Sheria hizi huendeshwa sambamba pamoja na Sheria na Kanuni za Kimataifa.

Ni vyema tukafahamu kuwa Sheria na Kanuni hizo humlazimu mwenye Meli, kujaza fomu maalumu ya maombi pamoja na Fomu za “DECLARATION OF VESSELS NON INVOLVEMENT WITH CRIMINAL ACTS OR OMISSIONS”; na ndipo hatua nyingine za kufanya uchunguzi wa historia ya meli kupitia International Maritime websites na vyanzo vingine, tangu Meli ilipotengenezwa hadi muda inapoomba usajili.

Uhakiki hufanywa pia kupitia mitandao mingine mikubwa mitatu inayotumika duniani kote kupata historia ya meli, Mitandao hiyo ni:

Fleet Moon; 
Maritime Traffic; na 

iii. Maritime-connector.

Baada ya ZMA ambayo ndio kisheria imeruhusiwa kusajili meli nje ya Tanzania, kujiridhisha na maelezo na taarifa zilizopatikana, maamuzi ya kusajili au kutosajili yanatolewa kupitia Idara ya Usajili.

Ndugu Waandishi wa Habari, kwa mujibu wa taratibu za Mkataba wa Kimataifa wa Kupambana na Usafirishaji wa Dawa za Kulevya, 1988 na Azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa 1970 (2011).

nchi zilizosajili Meli zinazokamatwa hutakiwa kutoa kibali kwa Walinzi wa Mwambao wa Bahari wa nchi husika, na kwa Meli hizi, tulitoa kibali kwa Jeshi la Mwambao wa Marekani na Jeshi la Mwambao wa Ugiriki kuzikamata na kuzipekua meli hizo.

Baada ya kupata taarifa za upekuzi hatua za haraka zilizochukuliwa upande wetu ni kufuta Usajili wa Meli hizo.

Ndugu Waandishi wa Habari, Tanzania vilevile ni mwanachama wa Mkataba wa Kimataifa wa Kupiga Vita Usafirishaji Haramu wa Dawa za Kulevya (United Nations Convention Against Illicit Traffic of Narcotic Drugs and Psychotropic Substance, 1988) na pia ni Mwanachama wa Mkataba wa Kimataifa wa Kupiga Vita

Usafirishaji Haramu wa Silaha (United Nations Protocol Against Illicit Manufacturing of and Trafficking in Arms, their Parts and Components and Ammunition, Supplementing the United Nations Convention Against Transnational Organized Crime, 2001).

Kwa mnasaba huu, tunapenda kutoa taarifa kuwa Tanzania imejidhatiti na imedhamiria kutekeleza majukumu yake yaliyoelezwa katika mikataba hiyo ya kimataifa, ikiwemo kushirikiana na mataifa mengine pamoja na mashirika ya kimataifa katika kupiga vita usafirishaji wa dawa za kulevya na silaha. Nyote ni mashahidi kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Awamu ya Tano imetangaza vita dhidi ya watu wote wanaojihusisha na dawa za kulevya na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vimekuwa vikifanya kazi usiku na mchana kuhakikisha vinatokomeza kabisa uhalifu huo.

Hivyo basi, taarifa ya kukamatwa kwa meli zenye bendera ya Tanzania zikisafirisha dawa za kulevya na silaha ni kinyume na Sheria za nchi yetu na zile za kimataifa. Taarifa hizi zimeleta mshtuko mkubwa ndani ya nchi yetu. hasa kwa kuwa Tanzania imejipambanua kupambana na maovu hayo kwa kutumia nguvu zote.

Ndugu Waandishi wa Habari, kufuatia taarifa hizo, Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliniagiza kuitisha kikao cha dharura baina ya viongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wale wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuzungumzia kadhia hiyo.
Jana Jumatano, tarehe 17 Januari 2018, Viongozi na Wataalamu wa pande zote mbili wakiongozwa na mimi mwenyewe na Mhe. Balozi Seif Ali Idi, Makamo wa Pili wa Rais, Zanzibar tulifanya kikao kilichojadili masuala haya kwa kina huko Zanzibar.

Ndugu Waandishi wa Habari, baada ya majadiliano ya kina kuhusu masuala haya, kikao kilibaini yafuatayo: 
Suala la Usajili wa Meli za Nje linafanywa na Nchi nyingiduniani; Kwa mfano katika Bara la Afrika 

nchi zinazofanya usajili wa kimataifa ni pamoja na Liberia, Komoro na Sierra Leone. Aidha, kwa Bara la Asia, kuna nchi za China na Singapore na kwa Amerika ya Kusini ni pamoja na Panama.

Ilibainika kwamba Wenye Meli hupendelea kusajili meli zao nje ya nchi zao kwa kukimbia uzito wa kodi na sheria zinazobana shughuli zao. 

Wakala aliyekuwa akifanya kazi hii kwa niaba ya ZMA na ambaye ameshavunjiwa Mkataba bado anaendelea kufanya usajili kwa kuiba Bendera ya Tanzania. 

Kutokana na hayo kikao kiliazimia yafuatayo: 
Kutoa taarifa na ufafanuzi wa kina kuhusu kadhia ya meli hizo kukamatwa na dawa za kulevya na silaha kwa umma wa Watanzania na dunia kwa ujumla ili kuondoa upotoshaji wa aina yoyote kwa kupitia vyanzo visivyo rasmi. Kwa sasa ndio natekeleza azimio hili; 

Kwa kuwa uendeshaji wa biashara hii unaonekana kuleta utata na kutia dosari kubwa kwa Taifa letu na kuharibu sifa njema za Nchi yetu, imeonekana haja ya kuunda kamati ya pamoja ya wataalam wa SMZ na SMT itakayoshirikisha vyombo vya ulinzi na usalama kwa ajili ya kupitiwa upya usajili uliokwishafanyika na kuzihakiki taarifa za meli zote zilizosajiliwa nchini mwetu, kuangalia mwenendo mzima wa usajili, na hatimaye kutoa mapendekezo na ushauri kwa Serikali; 

Kuanzisha utaratibu wa kuzifanyia uchunguzi wa kina (due diligence) meli zote mpya zitakazoomba usajili pamoja na wamiliki wake kwa kushirikisha vyombo mbalimbali vya Serikali vikiwemo vile vya ulinzi na usalama; 

iii. Kufanya mapitio ya sheria zetu, ili kuzipa nguvu zaidi taasisi zinazosimamia usajili wa meli. Wakati wa mapitio ya sheria, timu ya wataalam itaangalia kwa makini kodi zinazotozwa na mchango wake nchini ili zisiwe kivutio kwa meli zisizokidhi viwango kuomba usajili Tanzania;

Kuendelea kushirikiana na nchi nyengine kwa kuzipa ruhusa kukamata na kuzipekua meli zinazopeperusha bendera yetu wakati wote zinapohisiwa kuwa zinafanya uhalifu, au masuala ambayo haziruhusiwi kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni zinazokubalika kimataifa na wakati wa usajili. 


Asanteni kwa kunisikiliza.

No comments: