Thursday, April 30, 2015

NIC YATOA MSAADA WA VIFAA VYA ELIMU KWA WATOTO WENYE UONI HAFIFU KITUO CHA ALBINO BUHANGIJA SHINYANGA

Shirika la Bima la taifa leo limetoa msaada wa vifaa 34 vya kujifunzia darasani kwa watoto wenye uoni hafifu katika kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu wa ngozi(Albino),wasioona na wasiosikia cha Buhangija katika manispaa ya Shinyanga. Vifaa vilivyotolewa ni darubini kiona mbali(Telescope Monocular),Kikuza Maandishi cha Kusimamisha(Stand Magnifier) na Kikuza Maandishi cha Kuweka juu ya Maandishi( Dome Magnifier)-Picha zote na Kadama Malunde-Shinyanga
Ndani ya ofisi ya mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi Bungaja ambaye ndiye msimamizi mkuu wa kituo cha walemavu wa ngozi,wasioona na wasiosikia cha Buhangija katika manispaa ya Shinyanga,Mwalimu Peter Ajali (katikati),wa kwanza kushoto ni Meneja wa Shirika la Bima la taifa tawi la Shinyanga Halima Makange ,kulia ni Mstahiki meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez wakijadili jambo kabla ya kukabidhiana vifaa 34 vilivyotolewa na Shirika la Bima la taifa ikiwemo Darubini kiona mbali(Telescope Monocular),kikuza maandishi cha Kusimamisha(Stand Magnifier) na Kikuza Maandishi cha Kuweka juu ya Maandishi( Dome Magnifier)

Mtaalam wa Macho fani ya Uoni Hafifu kutoka hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga Dkt Ntoke Sospeter Wilson akiwaelekeza watoto hao namna ya kutumia Darubini Kiona mbali.
Watoto wakifanya majaribio kuhusu matumizi ya darubini kiona mbali.
Mtaalam wa Macho fani ya Uoni Hafifu kutoka hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga Dkt Ntoke Sospeter Wilson na Meneja wa Shirika la Bima la taifa tawi la Shinyanga Halima Makange wakiwaelekeza watoto hao namna ya kutumia Darubini kiona mbali.
Meneja wa Shirika la Bima la taifa tawi la Shinyanga Halima  Makange akimkabidhi  vifaa hivyo na kushikana mkono na msimamizi mkuu wa kituo cha Buhangija Peter Ajali
Mwalimu Peter Ajali akiwaonesha wanafunzi wake Darubini Kiona mbali.
Kulia ni Msimamizi mkuu wa kituo cha Buhangija Peter Ajali akiwaonesha wanafunzi wake moja ya darubini Kiona mbali.
Mtaalam wa Macho Fani ya Uoni Hafifu kutoka hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga Dkt Ntoke Sospeter akionesha baadhi ya vifaa hivyo na kueleza matumizi yake
Mstahiki meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez Mukadam akikagua vifaa hivyo wakati wa makabidhiano. Picha zote na Kadama Malunde-Shinyanga

Na Kadama Malunde-Shinyanga
*************
Shirika la Bima la Taifa leo limetoa msaada wa vifaa 34 vya kuwasaidia watoto wenye uoni hafifu katika kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu wa ngozi(Albino) cha Buhangija katika manispaa ya Shinyanga kutokana na idadi kubwa ya watoto hao kukabiliwa na changamoto ya uoni hafifu.


Vifaa vilivyotolewa  na Shirika la bima la taifa ni pamoja na      Darubini kiona mbali(Telescope Monocular),kikuza maandishi cha Kusimamisha(Stand Magnifier) na Kikuza Maandishi cha Kuweka juu ya Maandishi( Dome Magnifier).

Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo mbele ya mstahiki meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez Mukadam, meneja wa Shirika la Bima la Taifa tawi la Shinyanga Halima Makange alisema shirika hilo limeguswa na changamoto ya vifaa vya kujifunzia kwa wanafunzi wenye ulemavu wanaolelewa katika kituo hicho na kuamua kutoa msaada huo.

Alisema lengo la kutoa vifaa hivyo ni kuendeleza elimu kwa watoto hao kwani elimu ni jambo la msingi kwao pamoja na kwamba wanapata hifadhi katika kituo hicho.

“Kilichowaleta hapa watoto hawa ni elimu,tunahitaji kuwaendeleza kielimu ndiyo maana tumeleta vifaa hivi 34,ambavyo vitawasaidia kujifunzia darasani”,alisema Makange.

“Kwa niaba ya mkurugenzi wa shirika la bima la taifa Dar es salaam,nimeleta msaada huu kuungana na jamii kuwasaidia watoto wetu,ingawa vifaa hivi ni vidogo kwa kuviangalia lakini bei yake ni kubwa,tunamshukuru mkurugenzi wetu kwa kuona umuhimu wa kutoa vifaa hivi,naomba vitumike kama vilivyokusudiwa”,aliongeza Makange.


Kwa upande wake mstahiki meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez Mukadam alisema vifaa hivyo vitakuwa msaada mkubwa kwa wanafunzi wenye uoni hafifu waliopo katika kituo hicho cha walemavu.


“Kwanza niushukuru uongozi mzima wa shirika la bima la taifa kwa kunikaribisha kuja kukabidhi vifaa hivi,kwa niaba ya halmashauri ya manispaa ya Shinyanga tunashukukuru sana kwa msaada huu,naomba shirika liendelee kutoa ushirikiano kwa jamii kwani wanatambua nini jamii inahitaji,tutaendelea kushirikiana zaidi”,aliongeza Mukadam.

Naye  Mtaalamu wa Macho Fani ya Uoni Hafifu kutoka hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga Dkt. Ntoke Sospeter alisema vifaa hivyo vitatumika kuwaendeleza zaidi kimasomo watoto hao ili wafanane na watoto wengine wasiokuwa na tatizo la uoni hafifu.

“Mtoto  asiye ana tatizo la uoni hafifu anaona maandishi mapema zaidi,mwenye uoni hafifu anakuwa na uwezo mdogo wa kufikia maandishi,hivyo tunapompa kifaa tunamsaidia kufikia wenzake wanapofika”,alieleza Dkt Sospeter.

Kwa upande wake msimamizi mkuu wa kituo cha Kulelea watoto wenye Ulemavu wa ngozi(Albino),wasioona na wasiosikia Peter Ajali alilishukuru Shirika la bima la taifa kwa msaada huo kwani wamelenga kudumisha akili za watoto kimasomo.

Alisema asilimia kubwa ya watoto waliopo katika kituo hicho hawana uwezo wa kuona mbali hivyo vifaa vilivyotolewa vitawasaidia kuweza kuona maandishi kwa ufasaha zaidi.
Na Kadama Malunde-Shinyanga

No comments: