Friday, February 28, 2014

Kaya zaidi ya 5000 za manispaa ya Iringa kufikiwa na maji safi na salama

Katika kukamilisha ahadi na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011 – 2016), Serikali imejidhatiti kuwafikishia maji safi na salama wakazi wa zaidi ya kaya 5000 za Manispaa ya Iringa kufikia katikati ya mwaka huu wa fedha.

Hayo yalibainishwa na Naibu Katibu Mtendaji (Huduma za Jamii na Masuala ya Idadi ya Watu), Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri wakati wa ukaguzi wa miradi ya maendeleo inayodhaminiwa na serikali na wafadhili.

Bibi Mwanri alisema kuwa katika kutimiza Mpango wa huo wa Maendeleo Serikali inawekea mkazo katika Kuendeleza adhma yake ya utekelezaji wa miradi ya maji iliyoibuliwa katika Programu ya Matokeo Makubwa Sasa (BRN) hasa katika maeneo sugu yenye upungufu wa maji hasa maeneo ya vijijini ili kuweza kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuuendelea kuimarisha usimamizi vyanzo vya maji.

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Kaimu Mhandisi wa maji wa Mkoa wa Iringa, Mhandisi Kingazi William alisema kuwa kupitia Mpango huo wa Maendeleo wa Miaka Mitano zaidi ya vijiji 10 vya mkoa wa Iringa vitanufaika na miradi hiyo ya maji ambayo inagharimu zaidi ya milioni 600.

Maji ni eneo mojawapo la kipaumbele la kutekeleza Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano unaoratibiwa na kusimamiwa na Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango. Maeneo mengine.

ya vipaumbele yaliyoainishwa katika mpango ni pamoja na: miundombinu ya usafiri, nishati; kilimo; viwanda; maendeleo ya rasilimali watu; na huduma za jamii.
Mhandisi wa maji wa Manispaa ya Iringa, Taphali Ngwada (Kulia) akiwasilisha taarifa ya maendeleo ya mradi wa maji unaolenga kuzifikia zaidi ya kaya 5000 za manispaa hiyo wakati wa ukaguzi uliofanywa na wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango. Wataalam hao waliongozwa na Naibu Katibu Mtendaji (Huduma za Jamii na Masuala ya Idadi ya Watu), Bibi Florence Mwanri (Watatu Kulia mwenye koti jeusi) na Naibu Katibu Mtendaji (Uchumi Jumla, Prof. Longinus Rutasitara (Wapili Kulia).
Viongozi wa msafara wa wataalam wa ukaguzi wa miradi ya maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Naibu Katibu Mtendaji (Huduma za Jamii na Masuala ya Idadi ya Watu), Bibi Florence Mwanri (Kushoto) na Naibu Katibu Mtendaji (Uchumi Jumla, Prof. Longinus Rutasitara (Kulia) wakitaka ufafanuzi juu ya maendeleo ya mradi.
Kaimu Mhandisi wa maji wa Mkoa wa Iringa, Mhandisi Kingazi William (Kulia) akitoa ufafanuzi kuhusu maendeleo ya mradi wa maji unaolenga kuzifikia zaidi ya kaya 5000 za manispaa hiyo wakati wa ukaguzi uliofanywa na wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango.
Kaimu Mhandisi wa maji wa Mkoa wa Iringa, Mhandisi Kingazi William (aliyenyanyua mkono) akitoa ufafanuzi kuhusu maendeleo ya tanki la kuhifadhia maji kwa ajili ya mradi wa maji unaolenga kuzifikia zaidi ya kaya 5000 za manispaa ya Iringa.
Kamanda wa Kikosi cha Zimamoto wa Uwanja wa Ndege wa Iringa (Nduli) ambao ni wanufaika wa mradi wa maji unaolenga kuzifikia zaidi ya kaya 5000 za manispaa ya Iringa , Bw. Ranier Nyimbo (Mwenye Fulana nyeusi) akitoa maelekezo wakati wa ukaguzi uliofanywa na wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango kwenye uwanja huo.
Baadhi ya wanavijiji wa Nduli na Kigonzile kutoka manispaa ya Iringa wakichota maji katika bomba pekee linalopatikana katika mpaka wa vijiji hivyo. Adha hii itaisha mwezi Juni mwaka huu mara baada ya kukamilika kwa mradi wa maji unaolenga kuzifikia zaidi ya kaya 5000 za manispaa ikiwemo wanavijiji hawa.
Mhandisi wa maji wa Manispaa ya Iringa, Taphali Ngwada (Watatu Kulia) akiwaonesha wataalam kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango moja ya mabomba yatakayotumika kusambaza maji. PICHA NA SAIDI A. MKABAKULI

No comments: